SEKTA YA UVUVI YATAJWA KUWA NA MAENEO MAHSUSI YA KIMKAKATI, KUPITIA TEKNOLOJIA

Waziri wa Uchumi wa Buluu na Uvuvi katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Shaaban Ali Othman amesema Sekta ya Uvuvi inayo maeneo mahsusi ya kimkakati ili kukuza sekta hiyo kupitia teknolojia.
Akizungumza jijini Dar es Salaam (25.06.2025) wakati akizindua ripoti ya kitaalamu katika kutambua mahitaji ya teknolojia kwenye Sekta ya Uvuvi upande wa Bahari ya Hindi, ametaja maeneo hayo kuwa ni ufugaji wa samaki na kilimo cha mwani.
“Ripoti itasaidia mahitaji mahsusi ya kufahamu teknolojia ya namna gani inahitajika na kipindi gani ili wakulima wa mwani kuwa na uhakika wa mbegu zinazotumika, mahitaji ya soko na ufugaji wa mazao ya samaki kuwa na tija kwa wananchi.” amesema Mhe. Othman
Amefafanua kuwa kwa muda mrefu dunia imekuwa ikikabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi hivyo umuhimu wa tekonolojia ni dhahiri katika kufanya tathmini halisi ili kwenda na wakati.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede akimwakilisha Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji amesema ripoti hiyo imeangalia maeneo makubwa ikiwemo Sekta ya Uchumi wa Buluu ambayo ina samaki na mwani, huduma za usafirishaji na madini majini ambayo ni muhimu katika uzalishaji.
Dkt. Mhede ameongeza kuwa ripoti hiyo imebaini bado kunahitajika msukumo zaidi wa ushirikiano kati ya watunga sera na wachambuzi wa sera pamoja na sekta binafsi ambao ndiyo watumiaji wa sera hizo ili majibu ya teknolojia yazingatie uhalisia wa kitafiti.
Aidha, amesema kasi ya tekonolojia na tija lazima iendane sawa na ukuaji wa jamii ili mahitaji ya huduma mbalimbali hususan katika Sekta ya Uvuvi yasiwe na mapungufu.
Nao baadhi ya washiriki wa uzinduzi wa ripoti ya kitaalamu katika kutambua mahitaji ya teknolojia katika Sekta ya Uvuvi upande wa Bahari ya Hindi, wamepata fursa ya kutoa maoni ambapo wamesema ripoti hiyo ni muhimu katika kukuza Sekta ya Uvuvi hususan katika Uchumi wa Buluu.
Wamesema ni muhimu ripoti hiyo ikatumika vyema katika kufikia malengo na kuifanya Tanzania kufaidika na uchumi unaotegemea Bahari ya Hindi.
Umoja wa Mataifa una kitengo mahsusi ambacho kinafanya uchambuzi katika mataifa mbalimbali duniani juu ya uhalisia wa sekta za kiuchumi na mahitaji ya teknolojia ambapo Tanzania ni moja ya mataifa hayo.